Friday, July 27, 2012

WAZIRI MKUU AONGOZA MAZIKO YA MWALIMU WA BABA WA TAIFA

BUTIAMA.
WAZIRI MKUU, Mizengo Pinda na Mkewe Mama Tunu Pinda wameongoza Mamia ya waombolezaji  katika Maziko ya aliyemfundisha Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere katika  Shule ya Msingi Mwisenge Mjini Musoma,Mkoa wa Mara, Darasa la III na la IV Mwaka 1934, Marehemu James Irenge (120) katika mahame ya nyumbani kwao kijiji cha Busegwe Wilaya ya Butiama.

Akitoa salama za pole kwa familia ya Marehemu, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda  amemtaja Mzee James Irenge kuwa alikuwa na dhamani kubwa katika nchi hii kwani alimfundisha Baba wa Taifa na kwamba ndiye Mwalimu Mkuu wa Taifa hili kwani ndiye aliyemjengea misingi bora na kwamba ndiye aliyepanda mbegu bora kwa hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na kuwa kiongozi bora, mhadilifu na mchakapakazi.


Aliitaka familia kuwa na subira katika kipindi hiki kigumu ambapo wamepoteza mtu muhimu ambaye  walikuwa wanaendelea kupata baraka kutoka kwake na malezi bora.


Amesema kuwa wakati wa Ziara yake ya Mwaka jana Marehemu Irenge alimwomba msaada wa chakula ambapo kwa jitihada za serikali  zilitolewa  fedha kiasi cha Sh.300,000 kila mwezi na kwamba serikali haitaiacha familia bila kutoa msaada kwani Mjane wake bado yupo hivyo itaendelea kutoa huduma.


Aidha familia imeiomba Serikali kufuatilia kiinua mgongo na gharama za usafiri alizokuwa anadai Marehemu  Mwalimu Irenge kutoka Mkoa wa Geita kuja Musoma alikokuwa anafanya kazi kabla ya kustaafu kuanzia mwaka 1969 suala  ambalo ni la muda mrefu sasa ambapo fedha hizo apewe mjane wa Marehemu,Josephina Nyirembe ili zimsaidie.

Mwalimu James Irenge alifariki dunia nyumbani kwake  Mwisenge katika Manispaa ya Musoma Julai 21 mwaka huu kwa ugojwa wa moyo,Baba yake alifariki dunia majira ya 4 usiku.

Waziri Mkuu na Mkewe Mama Tunu Pinda waliweka mashada ya maua katika kaburi la Mwalimu James Irenge.


Katika Uhai wake Mwalimu Irenge aliwahi kuwa Mkaguzi Mkuu wa Elimu Kanda ya Ziwa, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Fulwe iliyoko Mkoa wa Geita na baada ya kustaafu Mwaka 1969/1970 alianzisha  Kijiji  cha  ujamaa cha Hiyayabuyaga-Geita  na mwaka 1980 aliendelea kuwa mkulima.Marehemu ameacha mjane, watoto 8 walioko hai, wajukuu  30, vitukuu 20 na vilembwe 8.

Katika uhai wake na kuhitimisha miaka 120 duniani, amefariki akiwa na meno yote kasoro jino moja ambalo aliwahi kuanguka na kulipoteza, pia alikuwa hatumii miwani kuona.



Katika maziko hayo viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali walihudhuria akiwemo Waziri  wa Nchi Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu,Steven Wasira ambaye pia ni  Mbunge wa Jimbo la Bunda, Mbunge wa Jimbo la Musoma Vicent Nyerere na  Mbunge wa Jimbo la Musoma Vijijini, Nimrode Mkono.

Ibada ya Maziko iliongozwa na Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Mara, Helkia Omindo.

Wednesday, July 25, 2012

MNARA WA MASHUJAA KUJEGWA MUSOMA.

MUSOMA.
Na: Ghati Msamba.



MKUU  wa Mkoa wa Mara, John Tuppa amewataka viongozi n awadau mbalimbali kuhakikisha kunajengwa Mnara wa kumbukumbu ya Mashujaa bila kupuuuza alama mbalimbali za mashujaa zilizopo ikiwemo ya mnara mdogo uliopo sasa.

 Aliyasema hayo katika maaddimisho ya siku ya mashujaa iliyofanyika kimkoa kwenye viwanja vya kanisa la Roman Cathoric (RC) Rwamlimi nje kidogo ya Manispaa ya Mji wa Musoma.

Alisema kuwa zoezi la ujenzi wa mnara mpya likisimamiwa na kuratibiwa ipasavyo mwakani, maadhimisho hayo yanaweza kufanyika katika Mnara mpya kuliko kwenda eneo jingine.

Aliongeza kuwa nia na madhumuni ya kuchagua Mnara mdogo kwa kuwa ina kumbukumbu ya kuanguka kwa ndege tatu za  kivita za Jeshi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ) zilizoanguka mwaka 1979.

“Hapa  pana nasaba kubwa na maadhimisho hayo kuliko kufanyia kwenye viwanja vya wazi, na kilichotoleta si dhehebu la dini bali ni alama ya Mnara yenye uhusiano na maadhimisho haya”

“Hatuna malipo yanayolingana na ushujaa waliouonyesha mashujaa wetu, hatuna.Tuendee kuwakumbuka na kuwaombea Amen”Alisema Tuppa.

Aliwataka wananchi wa Mkoa wa Mara kuendelea kufuata nyayo za mashujaa wetu, kulinda hazina za ujasiri, uzalendo, umoja na amshikamano walizotuachia na kutocheza amani iliyopo kwani haikujegwa siku moja  na kwamba  endapo tutadhubutu kuiachia itaondoka mara moja lakini itagharimu muda mwingi na jasho jingi kuirudisha.


Aidha maadhimisho hayo yanayanyika Julai 25, badala ya Septemba 1, 1964 ya kila mwaka  kwani julai 25,1979 ndiyo siku ambayo Taifa la Tanzania liliwapokea mashujaa rasmi waliokuwa wanarudi nchini wakitokea Uganda baada ya kumaliza kazi kubwa ya kishujaa ya kumng’oa nduli Idd Amin Dada, kwa mapokezi yaliyafanyika Nyakanazi  Mkoani Kagera na Septemba 1 ndiyo jeshi jipya la Wananchi wa Tanzania lilipoundwa baada ya jeshi la Zamani lililoridhiwa kutoka kwa wakoloni lilipovujwa.

Mkuu wa Mkoa huyo ameipongeza Parokia ya Ramwilimi na Kanisa Katoliki kwa kuutunza na kuulea Mnara huo na ushirikiano waliotoa kwa Serikali kila ilipohitajika kufanya shughuli  zake katika eneo hilo snajala na madhehebu mengine yalishiriki katika maadhimisho hayo bila kujali mahali maadhimisho  hayo yamefanyika.

Aidha ametaka wananchi kushiriki katika zoezi la sense ya watu na makazi la litakalofanyika Agosti 26 2012 na kuhudhuria kwa wingi ili kutoa maoni ya katiba Mpya pale itakapopita kupokea maoni juu ya katiba hiyo.


Kufanyika kwa Maadhimisho hayo kunatokana na agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Dk. Jakaya Kikwete kutoa maelekezo siku hii isiadhimishwe Mkoa wa Dar es Salaam pekee badala yake iadhimishwe kila Mkoa.

Monday, July 23, 2012

ALIYEMFUNDISHA BABA WA TAIFA, DRS LA I LA 11,
JAMES IRENGE(120) AFARIKI DUNIA.
MUSOMA.



ALIYEMFUNDISHA Mwalimu wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere darasa la
Kwanza na la Pili katika shule ya Msingi Mwisenge Mjini Musoma, Mkoa wa Mara, Mwaka 1934,James Irenge (120) amefariki dunia.

Mwalimu James Irenge alifariki dunia nyumbani kwake  Mwisenge katika Manispaa ya Musoma Julai 21 mwaka huu kwa ugojwa wa moyo na uzee.

Akizungumza na Uhuru nyumbani kwa marehemu jana, msemaji wa familia Josiah Irenge alisema kuwa Baba yake alifariki dunia majira ya 4 usiku akiwa nyumbani kwake na baadae mwili wake ukapelekwa kuhifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti kilichoko katika hospitali ya Mkoa mjini Musoma.

Akizungumza kwa majonzi alisema kuwa ameshangazwa na Madaktari ambao waliagizwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kumfanyia matibabu kutofika kabisa tangu Waziri huyo alifika mwaka jana Mjini Musoma kwa Ziara ya kikazi.

“Nakumbuka baba wakati wa uhai wake alimwomba Waziri Mkuu kuwa awe anapata matibabu na akaagiza  madaktari kumpatia matibabu lakini cha kushangaza tangu siku hiyo hawakuonekana na hivyo kuilazimu familia kuendelea kumuhudumia hadi mauti ilipompata”


Alisema Josiah na kuongeza kuwa anaishukuru serikali  kwa kuleta pesa za chakula ambazo pia aliomba kwa Waziri Mkuu ambapo zilipelekwa Sh.300,000 mara tatu  tangia mwaka jana.


Alisema wakati wa uhai wake  Mwalimu Irenge alikuwa anadai kiinua mgongo na gharama za usafiri kutoka Mkoa wa Geita kuja Musoma alikokuwa anafanya kazi kabla ya kustaafu kuanzia mwaka 1969 na kuiomba serikali kuingilia kati suala hilo ambalo ni la muda mrefu na fedha hizo apewe mjane wa Marehemu,Josephina Nyirembe ili zimsaidie.


Katika Uhai wake Mwalimu Irenge aliwahi kuwa Mkaguzi Mkuu wa Elimu Kanda ya Ziwa, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Fulwe iliyoko Mkoa wa Geita na baada ya kustaafu Mwaka 1969/1970 alianzisha  Kijiji  cha  ujamaa cha Hiyayabuyaga-Geita  na mwaka 1980 aliendelea kuwa mkulima,

.Marehemu ameacha mjane, watoto 12, wajukuu zaidi ya 30, vitukuu 20 na vilembwe 8.

Katika uhai wake na kuhitimisha miaka 120 duniani, amefariki akiwa na meno yote kasoro jino moja ambalo aliwahi kuanguka na kulipoteza, pia alikuwa hatumii miwani kuona.



 Aidha aliipongeza kampuni ya uhuru Publication kwa ufuatiaji  na umakini  wao katika kuhabarisha  Umma na hatimaye kusaidia kijana na marehemu ,Nassoro Irenge ( Bondia) ambaye alikuwa amepatwa na mkasa wa kesi isiyo yake nchini Afrika Kusini  na kurejea nchini jambo ambalo marehemu aliiomba asaidiwe na kufanikiwa.

Maziko yanatarajiwa kuwa  Alhamisi,julai 26 katika Mahame ya kijijini kwao Busegwe Wilaya ya Butiama, ambapo Waziri Mkuu Mizengo Pinda anatarajiwa kuongoza mamia ya waombolezaji katika maziko hayo.

Tuesday, July 17, 2012

MUSOMA.


JUMLA ya Wakufunzi wapatao 136 kutoka katika  Wilaya za Mkoa wa Mara, wamepata mafunzo ya Sensa ya watu na Makazi ya Mwaka 2012


Akifungua mafunzo hayo ya siku 12, yaliyoanza Julai 16 katika Ukumbi wa CCM Mkoa wa Mara, Mkuu wa Mkoa wa Mara, John Tuppa alisema zoezi la Sensa halitakwamisha shughuli za kiuchumi na kijamii kwani makarani wapo kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Alisisitiza kwa wananchi kwamba kuwa suala la Msingi ni kwamba kila mtu atakayelala nchini Agosti 25 kuamkia Agosti 26 ni lazima ahesabiwe mara moja tu.
“Ninawaomba wananchi wote mtoe ushirikiano wa kutosha kwa makarani wa Sensa ili kupata taarifa muhimu na sahihi kwa ajili ya mipango endelevu ya maendeleo ya nchi yetu”Alisema Tuppa.Na kuongeza “ kuweni marafiki kwa makarani hapo ili wafurahie kazi yao na matokeo yake yawe mazuri.


Aidha amevitaka vyombo vya dola, kamati za ulinzi na usalama za kila ngazi, Mgambo pamoja na vikundi vya ulinzi wa jadi chini ya dhana ya ulinzi shirikishi vichukue nafasi zao ili kuhakikisha zoezi la sensa linafanyika kwa usalama toka mwanzo hadi mwisho,sanjali na  ulinzi wa vifaa vya sensa.


Aliwataka kufuatilia mafunzo hayo kwa makini na usikivu wa hali ya juu ili hapo baadae wawe walimu wazuri watakaoendesha shughuli zote kwa usahihi na kwamba yapo maboresho makubwa yaliyofanywa katika madodoso na mfumo mzima wa utunzaji wa kumbukumbu kutokana na kukua kwa sayansi na teknolojia kwa kutumia teknojia ya Scanning ijuliknayo kama Optical Mark Reader(OMR)ambayo iliyotumika mwaka 2002.

Teknojia hiyo iliipa heshima kubwa nchi yetu katika Nyanja za kimataifa na kupelekea baadhi ya nchi za kiafrika kujifunza na kuchaguliwa kuwa mjumbe wa kamisheni ya Takwimu ya Umoja wa Mataifa.


Alitoa pongezi kwa Wilaya ya Tarime ambayo ilitoa ushirikiano wa kutosha katika jaribio la sense iliyofanyika katika kata za Matongo, Nyangoto A na B mwaka 2011, viongozi wa madhehebu ya dini, Vyama vya siasa, Mashirika yasiyo ya kiserikali, Taasisi mbalimbali za Umma na binafsi, vyama vya walemavu,Wazee, vyombo vya habari,Wabunge, Madiwani.


Aliwashukuru pia Wazee wa mila na Koo, viongozi wa serikali za Mitaa, viongozi n awatendaji ngazi ya Tarafa, Kata, vijiji hadi vitongoji na mitaa katika kazi kubwa ya kuhamasisha wananchi wa Mkoa wa Mara ili washiriki katika zoezi la Sensa.

Awali akisoma hotuba yake Mratibu wa Sensa Mkoa wa Mara, Ramadhan Mbega alisema kuwa mafunzo hayo yanashirikisha wakufunza wapatao 136 toka ngazi ya Mkoa na Halmashauri zote n akwamba uchaguzi wa wakufunzi hao ulifanywa kwa umakini wa hali ya juu na hivyo wana imani nao na kwamba wanatarajia kupata matokea chanya mwisho wa mafunzo hayo.


Alisema kuwa lengo kuu la mafunzo hayo ni kuwatayarisha watendaji wote watakaohusika katika zoezi la kukusanya taarifa kwa kufuata maelekezo kikamilifu kwa uelewa wa pamoja na kutoa ufahamu kwa wakufunzi jinsi ya kufundisha, kutafsiri na kutumia melekezo kwa makrani na wasimamizi, pamoj ana vifaa mbalimbali vya sensa.


Kufuatia sense zilizotangulia Mkoa wa Mara ulikuwa na watu 723,327 mwaka 1978,wanaume 118,476 wanawake 134,534 Mwaka 1988 wakikuwa watu 946,418 kati ya hao wanaume walikuwa 444,446 na wanawake 501,972, ambapo sensa ya mwaka 2002 walikuwa watu 1,362,397 wanawake wakiwa 713,690 na wanaume 649,707

WATU WANNE WAMEFARIKI MMOJA KWA KUJINYONGA

MUSOMA.



WATU wanne wamefariki dunia katika matukio mawili tofauti likiwemo la kujinyonga na ajali ya gari.

Akizungumza na blog hii, ofisini kwake Kamanda wa Polisi,Kamishna Mwandamizi wa Polisi (SACP), Absalom Mwakyoma alisema tukio la ajali lilitokea majira ya saa 9:40  Alasiri ,Julai 14 ambapo  watembea kwa miguu watatu walifariki dunia katika barabara iendayo Saragana- Kusenyi Suguti.

Alisema ajali hiyo ilihusisha  gari aina ya Jpsum yenye namba za usajili T 752 BQR likiendeshwa na Antony Kusaga(45) mwenye mali hiyo ambaye aliwagonga waenda kwa miguu, Asha Mwero(16) ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari ya Suguti Wilaya ya Musoma Vijijini ambaye alifariki dunia siku hiyio hiyo akipata matibabu katika hospitali ya Mkoa Musoma.

Aliwataja wengine wawili waliofia hapo hapo kuwa ni Nyakwesi Mwero ( 15) na Rebina Mwero (4) wote wakazi wa kijiji cha Suguti katika Wilaya ya Musoma Vijijini.

Alikitaja chanzo cha ajali kuwa inasadikiwa kuwa ni mwendo kasi aliokuwa nao dreva na kwamba dreva huyo alijisalimisha mwenyewe katika kituo cha polisi na kwamba tayari amefikishwa mahakamani.


Katika tukio jingine lilitokea Julai 17,asubuhi katika maeneo ya Mahakama kwenye nyumba ya Marehemu Dokta Emmanuel Magoti,  mtu mmoja ambaye bado hajajulikana jina lake mwenye jinsia ya kiume amekutwa akiwa amefariki baada ya kujinyonga ambapo mwili wake umepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospital ya Mkoa Musoma.


Amewataka wakazi wa Mji huo kwenda katika Chumba hicho kutambua mwili wa marehemu ili mwili wake ukazikwe vinginevyo utazikwa na serikali