Monday, July 23, 2012

ALIYEMFUNDISHA BABA WA TAIFA, DRS LA I LA 11,
JAMES IRENGE(120) AFARIKI DUNIA.
MUSOMA.



ALIYEMFUNDISHA Mwalimu wa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere darasa la
Kwanza na la Pili katika shule ya Msingi Mwisenge Mjini Musoma, Mkoa wa Mara, Mwaka 1934,James Irenge (120) amefariki dunia.

Mwalimu James Irenge alifariki dunia nyumbani kwake  Mwisenge katika Manispaa ya Musoma Julai 21 mwaka huu kwa ugojwa wa moyo na uzee.

Akizungumza na Uhuru nyumbani kwa marehemu jana, msemaji wa familia Josiah Irenge alisema kuwa Baba yake alifariki dunia majira ya 4 usiku akiwa nyumbani kwake na baadae mwili wake ukapelekwa kuhifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti kilichoko katika hospitali ya Mkoa mjini Musoma.

Akizungumza kwa majonzi alisema kuwa ameshangazwa na Madaktari ambao waliagizwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kumfanyia matibabu kutofika kabisa tangu Waziri huyo alifika mwaka jana Mjini Musoma kwa Ziara ya kikazi.

“Nakumbuka baba wakati wa uhai wake alimwomba Waziri Mkuu kuwa awe anapata matibabu na akaagiza  madaktari kumpatia matibabu lakini cha kushangaza tangu siku hiyo hawakuonekana na hivyo kuilazimu familia kuendelea kumuhudumia hadi mauti ilipompata”


Alisema Josiah na kuongeza kuwa anaishukuru serikali  kwa kuleta pesa za chakula ambazo pia aliomba kwa Waziri Mkuu ambapo zilipelekwa Sh.300,000 mara tatu  tangia mwaka jana.


Alisema wakati wa uhai wake  Mwalimu Irenge alikuwa anadai kiinua mgongo na gharama za usafiri kutoka Mkoa wa Geita kuja Musoma alikokuwa anafanya kazi kabla ya kustaafu kuanzia mwaka 1969 na kuiomba serikali kuingilia kati suala hilo ambalo ni la muda mrefu na fedha hizo apewe mjane wa Marehemu,Josephina Nyirembe ili zimsaidie.


Katika Uhai wake Mwalimu Irenge aliwahi kuwa Mkaguzi Mkuu wa Elimu Kanda ya Ziwa, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Fulwe iliyoko Mkoa wa Geita na baada ya kustaafu Mwaka 1969/1970 alianzisha  Kijiji  cha  ujamaa cha Hiyayabuyaga-Geita  na mwaka 1980 aliendelea kuwa mkulima,

.Marehemu ameacha mjane, watoto 12, wajukuu zaidi ya 30, vitukuu 20 na vilembwe 8.

Katika uhai wake na kuhitimisha miaka 120 duniani, amefariki akiwa na meno yote kasoro jino moja ambalo aliwahi kuanguka na kulipoteza, pia alikuwa hatumii miwani kuona.



 Aidha aliipongeza kampuni ya uhuru Publication kwa ufuatiaji  na umakini  wao katika kuhabarisha  Umma na hatimaye kusaidia kijana na marehemu ,Nassoro Irenge ( Bondia) ambaye alikuwa amepatwa na mkasa wa kesi isiyo yake nchini Afrika Kusini  na kurejea nchini jambo ambalo marehemu aliiomba asaidiwe na kufanikiwa.

Maziko yanatarajiwa kuwa  Alhamisi,julai 26 katika Mahame ya kijijini kwao Busegwe Wilaya ya Butiama, ambapo Waziri Mkuu Mizengo Pinda anatarajiwa kuongoza mamia ya waombolezaji katika maziko hayo.

No comments:

Post a Comment