MAELEZO
YA KIUTENDAJI YA MHESHIMIWA HAWA ABDUL RAHMANI GHASIA (MB), WAZIRI WA NCHI
OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA KUHUSU MAPITIO YA
KAZI MWAKA WA FEDHA 2011/12 NA MWELEKEO
WA KAZI KWA MWAKA WA FEDHA 2012/13
1.
Mheshimiwa
Spika, naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu
kunipa nguvu na kuniwezesha leo kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia,
nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa imani kubwa aliyoionesha
kwangu kwa kuniteua katika nafasi hii ya kuwa Waziri wa Nchi, katika Ofisi ya
Waziri Mkuu ili nishughulikie Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Naahidi
kufanya kazi kwa uwezo wangu kadri mungu atakavyonijalia.
2.
Mheshimiwa
Spika, naomba nitumie fursa hii pia kumshukuru Mheshimiwa
Mizengo Peter Pinda (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
hotuba nzuri ya Mwelekeo na Malengo ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka
wa fedha 2012/13. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Stephen Masato Wasira (Mb), kwa
hotuba ya Taarifa ya Hali ya Uchumi kwa mwaka 2011/12 na Mpango wa Maendeleo wa
Taifa kwa mwaka 2012/13. Pia nampongeza Mheshimiwa Dk. William Mgimwa (Mb), Waziri wa Fedha kwa
kuteuliwa kushika wadhifa huo na nimpongeze vilevile kwa hotuba aliyotoa kuhusu
Mapendekezo ya Serikali ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2012/13. Hotuba zote zilizotangulia zimeonesha
mwelekeo wa utekelezaji wa shughuli za Serikali kwa mwaka 2012/2013.
3.
Mheshimiwa
Spika, napenda kukushukuru wewe Mheshimiwa Spika na
Mheshimiwa Naibu wa Spika kwa uongozi imara na madhubuti katika Bunge
hili. Aidha, namshukuru kwa namna ya
pekee Naibu Waziri Mheshimiwa Aggrey D. J. Mwanri (Mb) wa Siha,
anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Majaliwa Kasimu
Majaliwa (Mb) wa Ruangwa, anayeshughulikia
Elimu
chini ya OWM-TAMISEMI, Katibu Mkuu Bw.
Hussein A. Kattanga, Naibu Makatibu
Wakuu Bw. Jumanne A. Sagini, Bw. Alphayo J. Kidata,
Wakurugenzi na Watumishi wa OWM-TAMISEMI ambao kwa kipindi kifupi nilichofanya
nao kazi wamenipa ushirikiano wa kutosha hivyo, ni imani yangu tutafanikisha
kuyatekeleza majukumu ya ofisi kwa manufaa ya Watanzania wote. Niwashukuru Wakuu
wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wote wa Mikoa na Wilaya, Wakurugenzi
wa Halmashauri na Mabaraza ya Madiwani, wote kwa pamoja nawaahidi ushirikiano.
4.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuwapongeza wafuatao kwa kuteuliwa na
Mheshimiwa Rais kuwa Mawaziri kama ifuatavyo: Mhe. Dkt. Harrison George
Mwakyembe (Mb); Mhe. Dkt. Fenella Ephraim Mukangara (Mb); Mhe. Balozi Khamis
Sued Kagasheki (Mb); Mhe. Prof. Sospeter Mwijarubi Muhongo (Mb); Mhe. Mhandisi
Christopher Kajoro Chiza (Mb); Mhe. Dkt. Abdallah Omari Kigoda (Mb).
5.
Mheshimiwa
Spika, aidha, napenda kuwapongeza wafuatao kwa kuteuliwa kuwa Naibu
Mawaziri katika Wizara mbalimbali, Mhe. Janet Zebedayo Mbene (Mb); Mhe. Saada
Mkuya Salum (Mb); Mhe. Dkt. Seif Suleiman Rashid (Mb); Mhe. George Boniface
Simbachawene (Mb); Mhe. January Yusuf Makamba (Mb); Mhe. Dkt. Charles John
Tizeba (Mb); Mhe. Amos Gabriel Makalla (Mb); Mhe. Angela Jasmine Kairuki (Mb);
Mhe. Stephen Julius Maselle (Mb); na Mhe. Mhandisi Dkt. Binilith Satano Mahenge
(Mb.).
6.
Mheshimiwa
Spika, napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Mhe. Musa Azan
Zungu (Mb) wa Ilala kwa kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge. Kadhalika, nampongeza
Mhe. James Mbatia (Mb) kwa kuteuliwa na Mhe. Rais kuwa Mbunge, na Waheshimiwa
Dkt. Dalali Kafumu, Joshua Nasari kuchaguliwa kuwa Wabunge katika Majimbo yao na
Mhe. Cesilia Pareso kuwa Mbunge wa Viti Maalum.
7.
Mheshimiwa
Spika, nitumie fursa hii pia kutoa pole kwa familia za Wabunge
wenzetu waliopoteza maisha baada Bunge la Bajeti la mwaka 2011/2012. Wabunge hao ni Marehemu Jeremiah Sumari
aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki na Marehemu Regia Mtema
aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum. Tunaomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu
mahali pema peponi na awajalie ndugu jamaa na marafiki wa marehemu moyo wa subira.
8.
Mheshimiwa
Spika, napenda kutoa shukrani za dhati kwa Kamati ya Katiba,
Sheria na Utawala chini ya Uongozi wa Mwenyekiti Mheshimiwa Pindi Hazara Chana
(Mbunge wa Viti Maalum - CCM) na Makamu Mwenyekiti Mhe. John Paul Lwanji (Mbunge
wa Manyoni Magharibi) kwa kuichambua bajeti ya ofisi yetu na kutupa maoni na
ushauri ambao unaendelea kutujenga katika utendaji wetu wa kazi, nawashukuru
sana. Tutayachukua maoni na ushauri walioutoa kwa uzito unaostahili na
kuufanyia kazi.
9.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuwashukuru wananchi wa Mtwara Vijijini kwa
mshikamano na ushirikiano wanaonipatia katika majukumu yangu ya ubunge na
uwaziri wa Nchi, OWM-TAMISEMI. Naahidi
kuendelea kuwatumikia kwa kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia ili kwa pamoja
tufanikishe shughuli za kujiletea maendeleo katika Jimbo letu.
Utekelezaji wa Majukumu
kwa Mwaka wa Fedha 2011/12 na Mwelekeo kwa Mwaka wa Fedha 2012/13
Utawala Bora
10. Mheshimiwa Spika, Serikali
za Mitaa ndio mhimili mkubwa wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika
lengo zima la kuhakikisha yanakuwepo maendeleo endelevu katika nchi yetu. Upelekaji wa madaraka kwa wananchi unapitia katika
Mamlaka za Serikali za Mitaa na ndiyo maana Serikali za Mitaa na ushirikishwaji
wa Wananchi katika mchakato wa maendeleo vimetambuliwa katika Katiba na Sheria
za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ufafanuzi wa dhana ya kupeleka madaraka kwa
wananchi umeelezwa kwa kina zaidi katika Sera ya Uboreshaji wa Mfumo wa
Serikali za Mitaa ya mwaka 1998 (The Policy Paper on Local Government Reform of
1998). Katika Sera hii, Mamlaka za Serikali za Mitaa zinapewa uhuru (autonomy)
wa kufanya maamuzi mbalimbali yanayohusu utoaji wa huduma kwa wananchi walio
katika mamlaka hizo kwa kuwashirikisha wananchi katika kujiletea maendeleo na
ustawi wao kwa ujumla. Mamlaka za Serikali za Mitaa zinatakiwa kuutumia uhuru
huo kwa kuzingatia Katiba na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
endapo zitakwenda kinyume chake, Serikali Kuu inao wajibu wa Kikatiba na
Kisheria kuingilia kati (intervene) na kuchukua hatua dhidi ya mamlaka hizo.
11. Mheshimiwa
Spika, Mpango wa Uboreshaji wa Mfumo wa Serikali za Mitaa umetekelezwa kwa awamu
mbili. Awamu ya Kwanza ilianza kutekelezwa mwaka 1998 hadi 2008 na Awamu ya Pili
imeanza kutekelezwa mwaka 2009 na utakamilika mwaka 2014. Katika awamu ya pili Mikoa yote imepatiwa Wataalam
Washauri watakaosaidia kujenga uwezo wa ngazi hii ili kuweza kuzishauri na
kuzisimamia kwa karibu Mamlaka za Serikali za Mitaa. Wataalam hawa watafanya kazi
kwa karibu na Makatibu Tawala Wasaidizi katika Sekretarieti za Mikoa katika
kuimarisha masuala ya fedha na rasilimali watu katika Mamlaka za Serikali za
Mitaa. Ni matarajio yetu kwamba baada ya muda, wataalam wote walio katika
Sekretarieti za Mikoa watakuwa wamejengewa uwezo wa kusimamia shughuli hizo.
12. Mheshimiwa
Spika, katika kipindi hiki Halmashauri
62 zimepatiwa magari ili kuwezesha
vitengo vya Ukaguzi wa Ndani kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Nyenzo hii
ya usafiri itawawezesha kukagua shughuli mbalimbali zinazotekelezwa katika
ngazi za chini za Halmashauri na hivyo kubaini thamani ya fedha katika miradi
inayotekelezwa. Aidha, Mikoa yote
imepatiwa magari ambayo yatatumiwa na Wataalam waliopelekwa katika ngazi hiyo
pamoja na wale wa sehemu ya Usimamizi wa Serikali za Mitaa ili kuwawezesha
kuzifuatilia kwa karibu Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizo katika Mikoa yao.
13. Mheshimiwa
Spika, ili Madiwani waweze
kutekeleza majukumu yao vema umeandaliwa utaratibu wa kuwakopesha
vyombo vya usafiri kupitia Benki. Tayari makubaliano yameshafikiwa kati ya Serikali
na NMB ili kuwawezesha Madiwani kupata vyombo vya usafiri. Baadhi ya Madiwani
wameanza kufaidika na utaratibu huu.
14. Mheshimiwa Spika, Waweka
Hazina katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wamejengewa uwezo kwa kupatiwa
mafunzo ya viwango vya Kimataifa vya Uhasibu katika Sekta ya Umma
(International Public Sector Accounting Standards (IPSAS)). Hivyo, ni mategemeo yetu kwamba mfumo huu utawasaidia
katika kutekeleza majukumu waliyokabidhiwa ya kusimamia vizuri fedha za Serikali
na kutoa taarifa zilizo sahihi kwa wakati unaotakiwa.
15. Mheshimiwa Spika, katika
kutekeleza shughuli zinazohusiana na uboreshaji wa uendeshaji wa Mabaraza ya
Kata, OWM-TAMISEMI ilimteua Mtaalam
Mshauri ambaye alipewa kazi ya kupitia Sheria na nyaraka mbalimbali zinazohusu
uendeshaji wa Mabaraza ya Kata na kupendekeza namna bora ya kuboresha utendaji
kazi wa Mabaraza hayo kwa kuzingatia mabadiliko yaliyotokea hadi sasa. Baadhi
ya matatizo yaliyoibuliwa na Mtaalam Mshauri katika taarifa yake ni pamoja na malipo
na posho kwa Wajumbe wa Baraza la Kata; uwezo na sifa za Wajumbe wa Mabaraza ya
Kata; mafunzo kwa wajumbe wa Baraza la Kata; ukosefu wa vitendea kazi; kutekeleza
majukumu ya Kimahakama zaidi kuliko ya usuluhishi; Mabaraza hayo kuwepo chini
ya Mamlaka tatu tofauti yaani chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa
(OWM-TAMISEMI), Baraza la Ardhi na Nyumba la Wilaya ambalo lipo chini ya Wizara
ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi na Mahakama Kuu.
16. Mheshimiwa Spika,
Changamoto zilizojitokeza katika taarifa hiyo zilijadiliwa na wadau mbalimbali
na hatimaye maoni na mapendekezo ambayo yaliwasilishwa Serikalini. Maoni na
mapendekezo hayo yanafanyiwa kazi na Serikali kwa kushirikiana na Tume ya
Kurekebisha Sheria.
Watumishi wa Mamlaka za Serikali za
Mitaa
17. Mheshimiwa Spika, ili
kuimarisha utendaji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, Serikali imekuwa
ikichukua hatua kwa watumishi wanaotuhumiwa kwa makosa mbalimbali. Kuanzia
mwaka 2009/10 hadi Machi, 2011/12, Wakurugenzi wa Halmashauri wapatao 24
walichukuliwa hatua za kinidhamu, kati yao 8 walivuliwa madaraka, 11 walipewa
onyo, 3 wamepumzishwa kazi na 2 wamesimamishwa kazi na kesi ziko
mahakamani. Aidha, Wakuu wa Idara 74 wa
Halmashauri mbalimbali wamechukuliwa hatua za kinidhamu kutokana na tuhuma
zinazowakabili.
Kujenga Uwezo wa Sekretarieti za Mikoa
18. Mheshimiwa Spika, Ofisi yangu imetoa mafunzo
kwa viongozi wa Sekretarieti za Mikoa ili kuwakumbusha majukumu yao kwa lengo
la kuboresha utendaji wa kazi. Mafunzo
yaliyotolewa ni pamoja na Maandalizi ya Mipango na Bajeti kwa Makatibu Tawala
Wasaidizi 75 kutoka Mikoa 21. Mafunzo
hayo yalilenga kuwapa uelewa zaidi katika kuandaa Mipango, Bajeti na Taarifa za
Mikoa yao. Makatibu Tawala wa Mikoa 21
walipata mafunzo hayo katika Chuo cha Serikali za Mitaa Hombolo ambapo dhumuni
kubwa lilikuwa ni kuwajengea uwezo wa kiutendaji ili kuwawezesha kuzisimamia
Mamlaka za Serikali za Mitaa katika maeneo yao.
19.
Mheshimiwa
Spika, kujenga uwezo wa Sekretarieti za Mikoa ni pamoja na
kuimarisha utendaji wa Maafisa Tarafa.
Mkakati uliopo ni kuhakikisha kuwa Maafisa Tarafa wanapata vitendea kazi
hususan vyombo vya usafiri na ofisi. Aidha,
nafasi wazi za Maafisa Tarafa 145 tayari zimepata kibali cha ajira na mchakato
wa kuwaajiri unaendelea.
20. Mheshimiwa Spika, Ofisi yangu imeendelea
kuzifanyia mapitio Sheria mbalimbali ili ziweze kuendana na mabadiliko
yanayojitokeza katika uendeshaji wa shughuli za Mamlaka za Serikali za Mitaa na
Sheria ya Tawala za Mikoa namba 19 ya mwaka 1997. Mapitio yatakapokamilika
yatawasilishwa mbele ya Bunge lako tukufu. Lengo kubwa ni kuimarisha utendaji wa
Mamlaka za Serikali za Mitaa na Sekretarieti za Mikoa.
Mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa
21. Mheshimiwa
Spika, makisio ya mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha
2010/11 makadirio yalikuwa shilingi bilioni 173.1 na makusanyo halisi yalikuwa
shilingi bilioni 158.3 sawa na asilimia 92. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2011/12 makadirio
yalikuwa shilingi bilioni 350.5. Hadi kufikia Machi 2012 zimekusanywa shilingi
bilioni 142 .8 sawa na asilimia 40.7.
22. Mheshimiwa Spika, changamoto
kubwa katika Halmashauri ni kujiwekea makadirio kidogo katika ukusanyaji
mapato. Ili kuondoa tatizo hili Ofisi yangu imeanza kuandaa mikakati ya kusaidia kuimarisha
ukusanyaji wa mapato. Vikao vya
kitaalamu vya uchambuzi wa mipango na bajeti za kila chanzo na ushahidi wa
takwimu za walipa kodi na vitu vinavyolipiwa kodi (Tax Payers na Tax Objects)
vimefanyika. Taarifa hizo muhimu zitatumika pamoja na taarifa za utafiti
unaotarajiwa kufanywa na wataalamu washauri katika kuboresha mifumo ya
ukusanyaji mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa
Hesabu za Serikali
23. Mheshimiwa
Spika, taarifa ya ukaguzi wa hesabu
za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha ulioishia tarehe 30 Juni
2011 iliwasilishwa Bungeni tarehe 12 Aprili 2012. Kwa mara ya tatu mfululizo,
hesabu hizi ziliandaliwa kwa kuzingatia viwango vya kimataifa vya uhasibu kwa Sekta
ya Umma (IPSAS). Kwa ujumla, matokeo ya
ukaguzi wa hesabu hizo yanaonesha kuwa bado kuna kazi ya ziada ya kufanya ili
kuwa na utendaji ulioimarika katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
24. Mheshimiwa
Spika, taarifa ya Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) inaonesha kuwa kiwango cha utendaji
katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kinaendelea kuimarika. Hii inatokana na
ukweli kwamba; kumekuwa na ongezeko la Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopata
hati zinazoridhisha (safi) kutoka 66 (48.9%) mwaka 2009/10 mpaka hati 72 (54%)
mwaka 2010/11. Aidha, Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopata hati zenye shaka zimepungua
kutoka 64 (48.1%) mwaka 2009/10 mpaka hati 56 (42%) Mwaka 2010/11. Vilevile, kumekuwa
na ongezeko la Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopata hati zisizoridhisha
(chafu) kutoka 4 (3%) mwaka 2009/10 mpaka 5 (4%) mwaka 2010/11.
25. Mheshimiwa
Spika, katika taarifa ya ukaguzi
huo, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali amebainisha sababu za
Mamlaka za Serikali za Mitaa kupata hati zenye shaka au zisizoridhisha kama
ifuatavyo; Kutotolewa kwa mafunzo ya
kutosha ya kuandaa taarifa za fedha kwa kutumia viwango vya kimataifa vya
uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSASs) na hivyo kuandaliwa kwa taarifa za fedha
zisizo sahihi; Kuwepo kwa watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wanaokiuka maadili ya kazi zao na kujihusisha
na ubadhirifu wa fedha za Halmashauri na hata kula njama na watumishi wa Benki na
udhaifu wa mifumo ya udhibiti wa ndani.
26. Mheshimiwa
Spika, ninamshukuru Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa kuainisha vyanzo vya mapungufu
yaliyoonekana wakati wa ukaguzi. Hii imetusaidia kuanza kuyafanyia kazi ili
kuzuia kujirudia kwa hali hii. Eneo tunalolipa kipaumbele ni kuimarisha mifumo
ya udhibiti wa ndani na usimamizi kwenye ngazi za Mamlaka za Serikali za Mitaa
na Mikoa.
27. Mheshimiwa
Spika, ili kuzipa uwezo
Halmashauri kusimamia fedha kwa ufanisi, matumizi ya mfumo wa Epicor 9.05 katika
mfumo wa “Intergrated Financial Management System (IFMS)” utaanza kutumika kwa
Halmashauri zote nchini mwaka wa fedha 2012/13. Aidha, mwezi Mei, 2012 Ofisi ya
Waziri Mkuu, TAMISEMI imefanya Mkutano wa kazi uliowashirikisha Makatibu Tawala
wa Mikoa yote, Wakurugenzi wa Halmashauri zote, Waweka Hazina wa Halmashauri
zote pamoja na wataalam wengine kutoka ngazi ya Mkoa kwa ajili ya kutafuta
suluhisho la kudumu la dosari na mapungufu yanayoendelea kujitokeza katika
taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali. Moja ya maazimio muhimu
ya Mkutano huo ni kwamba kuanzia sasa makosa yanayotokana na uzembe na uwezo mdogo
wa kusimamia kazi hautavumiliwa. Kila Katibu Tawala wa Mkoa atawajibika kwa
kutokuchukua hatua zinazolenga kuongeza ufanisi na uwajibikaji katika
Halmashauri chini ya Mkoa anaoongoza. Kadhalika Mkurugenzi wa Halmashauri
atapimwa kwa kigezo cha uwajibikaji kutokana na tathmini mbalimbali ikiwemo
taarifa ya ukaguzi, kuweka kwenye mbao za matangazo taarifa za miradi
inayotekelezwa katika Halmashauri pamoja na fedha zote zilizopokelewa kwa ajili
ya miradi hiyo.
28. Mheshimiwa
Spika, katika kuhakikisha kunakuwa
na uzingatiaji wa viwango vya kimataifa vya uhasibu kwa Sekta ya Umma (IPSASs)
na kunakuwa na usahihi wa taarifa za hesabu zinazoandaliwa na Mamlaka za
Serikali za Mitaa, Serikali itaendelea kutoa mafunzo yanayotakiwa kwa wahasibu
katika ngazi zote zinazohusika. Aidha, Serikali itahakikisha kuwa watumishi
wote watakaobainika kuhusika na ubadhirifu, wizi na kuzisababishia hasara
Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kutowajibika ipasavyo, wanachukuliwa hatua ..kwa
mujibu wa kanuni,sheria na taratibu.
29. Mheshimiwa
Spika, pamoja na taarifa hizo
napenda kuzipongeza Halmashauri 11 ambazo zimeendelea kupata hati
zinazoridhisha (hati safi) kwa kipindi cha miaka minne (4)
mfululizo; Halmashauri hizo ni za Wilaya za Mufindi,
Biharamulo, Missenyi, Siha, Nachingwea, Serengeti, Kyela, Maswa, Singida na
Manispaa ya Shinyanga. Vilevile,
napenda kuupongeza uongozi wa Mkoa wa Mtwara kutokana na Halmashauri zote za
Mkoa huo kupata hati zinazoridhisha.
Mfuko wa
Barabara za Serikali za Mitaa
30. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha 2011/12
kiasi cha shilingi bilioni 94.02 kutoka katika Mfuko wa barabara zilitengwa kwa
ajili ya matengenezo ya barabara za Halmashauri. Hadi kufikia mwezi Machi, 2012
jumla ya shilingi bilioni 73.7 zilikuwa zimepokelewa na kupelekwa kwenye
Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara, pamoja
na miradi mikubwa kupitia fedha za maendeleo ambazo ni asilimia 10 ya bajeti ya
Mfuko wa Barabara zinazotolewa kwa OWM-TAMISEMI.
31. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2012/13 kiasi cha shilingi bilioni 128.9 kinategemewa kutoka
kwenye Bodi ya Mfuko wa Barabara kwa ajili ya kutekeleza kazi mbalimbali.
Mfumo wa Kupeleka Ruzuku ya Maendeleo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa (LGDG)
32.
Mheshimiwa Spika, Mfumo wa Kuzipatia Mamlaka za Serikali za Mitaa ruzuku ya maendeleo
ulianza kutekelezwa katika mwaka wa fedha wa 2004/05. Mfumo huu ndio unaotumika
katika kugawa ruzuku ya maendeleo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa
kuzingatia uwazi na usawa. Kupitia Mfumo huu, tathmini ya Mamlaka za Serikali
za Mitaa hufanyika kila mwaka na ruzuku ya maendeleo hupelekwa katika Mamlaka
hizo kulingana na jinsi zilivyofuzu vigezo vilivyowekwa. Ruzuku ya kujenga
uwezo hutolewa kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa zote kwa ajili ya kujiimarisha
kiujuzi na maarifa kwenye maeneo ambayo Mamlaka hizo zitakuwa zimebaini kuwa na
upungufu.
33. Mheshimiwa
Spika, Mfumo huu ulifanyiwa tathmini mwezi Septemba 2011. Mojawapo ya
mapendekezo yaliyotolewa katika tathmini hii ni kufanya mapitio ya vigezo vya
tathmini, kiwango cha ruzuku na namna ya kupata ruzuku ya maendeleo na ya
kujenga uwezo. Kutokana na mapendekezo haya, utaratibu mbadala unaandaliwa
ambao utatumika kupima Mamlaka za Serikali za Mitaa. Utaratibu mbadala
unaopendekezwa ni wa kuzitumia Sekretarieti za Mikoa katika upimaji wa awali wa
Mamlaka za Serikali za Mitaa. Mamlaka za
Serikali za Mitaa ambazo zitakuwa zimeshindwa kufuzu, ufuatiliaji utafanywa na timu
ya wataalam ili kubaini chanzo cha mapungufu pamoja na mbinu za kuondokana na
mapungufu hayo. Hata hivyo, taarifa ya Mdhibiti
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali huzingatiwa wakati wa kufanya maamuzi ya
Mamlaka za Serikali za Mitaa zitakazopata Ruzuku ya Maendeleo na Kujenga Uwezo.
34. Mheshimiwa
Spika, hadi kufikia Aprili 2012, jumla ya shilingi
bilioni 106.6 zimepelekwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia Mfumo huo
zikiwa ni ruzuku isiyo na masharti.
Aidha, kwa upande wa Sekta ya Kilimo jumla ya shilingi bilioni 59.8
zilikuwa zimepelekwa kwa ajili ya ruzuku ya maendeleo ya kilimo na shilingi bilioni
43.3 zilipelekwa kwa ajili ya ruzuku ya maendeleo ya maji vijijini. Vilevile shilingi bilioni 80.9 za Mfuko wa
Pamoja wa Sekta ya Afya ambazo ni asilimia 100 zimetolewa na kupelekwa katika
Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Mradi wa
Uboreshaji wa Miundombinu ya Miji Tanzania (TSCP)
35. Mheshimiwa
Spika, Mradi wa uboreshaji wa
miundombinu katika Miji Tanzania ni matokeo ya makubaliano kati ya Serikali ya
Tanzania, Benki ya Dunia na Serikali ya Denmark. Mradi ulizinduliwa rasmi
Oktoba, 2010 na umepangwa kutekelezwa hadi mwaka 2014/15. Madhumuni ya mradi
huu ni kuziwezesha Halmashauri nane (8) zinazohusika na utekelezaji wa mradi
huu, kuboresha miundombinu na utoaji wa huduma za jamii katika Miji. Mamlaka
hizi ni Jiji la Mwanza, Tanga na Mbeya; Manispaa za Arusha, Dodoma, Kigoma
Ujiji, Mtwara Mikindani na Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma. Hadi
Machi, 2012, shilingi 21,520,034,150.00 (Kati ya shilingi 49,807,534,150.00
zilizotengwa) zilikuwa zimetolewa kwenye Halmashauri na Mamlaka ya Ustawishaji
Makao Makuu Dodoma kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi mbalimbali. Kiasi kilichobakia kitaendelea kutolewa kadri
utekelezaji unavyoendelea.
36. Mheshimiwa
Spika, mbali ya fedha za ujenzi
wa miundombinu, kiasi cha shilingi 4,068,292,750.00 kimeshapelekwa kwenye
Mamlaka zinazotekeleza mradi huu kwa ajili ya kujenga uwezo katika maeneo
mbalimbali katika Mamlaka hizo. Maeneo hayo ni kama vile Idara za Mipango Miji
ambapo yamefanyika mafunzo ya Geographical Information Systems (ARC–GIS) pamoja
na ununuzi wa mfumo huo (ARC–GIS software). Vilevile, Wizara ya Ardhi imepewa
kandarasi ya kurekebisha picha za Satelite (Rectification and Digitization of
satelite image) na kazi hiyo inaendelea kutekelezwa katika maeneo ya mradi.
Mradi wa
Kuimarisha Halmashauri za Manispaa 11 na Miji 7
37. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha
2012/13 Serikali itaanza utekelezaji wa Mradi wa kuimarisha miundombinu pamoja
na uwezo wa kutoa huduma za jamii katika Halmashauri za Manispaa 11 na Miji 7
(Urban Local Government Strengthening Programme). Manispaa zinazohusika ni
Morogoro, Moshi, Iringa, Bukoba, Shinyanga, Singida, Musoma, Sumbawanga, Songea,
Lindi na Tabora. Miji inayohusika ni Babati, Njombe, Korogwe, Mpanda, Kibaha,
Geita na Bariadi. Mradi utatekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia
2012/13 hadi 2016/17. Mradi utagharimu kiasi cha dola za kimarekani milioni 175
ikiwa ni mkopo kutoka Benki ya Dunia.
Kati ya fedha hizo, dola milioni 160 zitagawiwa katika Halmashauri
husika kwa ajili ya kuimarisha miundombinu ya aina mbalimbali kulingana na
mipango ya Halmashauri hizo. Fedha zinazobaki yaani dola milioni 15 ni kwa
ajili ya uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa mradi huo.
TEHAMA
38. Mheshimiwa Spika,
Ofisi yangu imeendelea kuhakikisha kuwa taarifa sahihi zinapatikana katika
ngazi zote za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na kuwezesha utoaji wa
huduma kupitia Serikali Mtandao. Miundo
ya Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa imetengenezwa kwa
kuzingatia mahitaji ya TEHAMA na hivi sasa vimeanzishwa vitengo vya TEHAMA
katika ngazi hizo.
39. Mheshimiwa Spika,
ili kuboresha mawasiliano tumefunga vifaa vya mawasiliano kwa ajili ya “video conferencing”
katika kila Sekretarieti ya Mkoa. Ofisi inaendelea kujenga uwezo kwa kutoa
msaada wa kiufundi ili Mikoa iweze kutoa huduma ya kiufundi ya TEHAMA katika
Mamlaka za Serikali za Mitaa yaani Dawati la Usaidizi la TEHAMA. Aidha, Ofisi imeanzisha
“Computer Laboratory” kwa ajili ya kufundisha watumishi wake katika ngazi zote kuhusu
mifumo mbalimbali inayotumika katika utendaji wa kazi.
40. Mheshimiwa Spika,
mifumo ambayo imeshafanyiwa kazi katika ngazi zote za Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa ni ifuatayo:- Tovuti za Sekretarieti za Mikoa, mfumo wa barua pepe,
mfumo wa “Intergrated Financial Management System,” “Planrep” na Mfumo wa
Usimamizi wa Rasilimali Watu wa Mamlaka za Serikali za Mitaa (LGHRIS) ambao
ulitengenezwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa Ufadhili wa “Intra-Health
International”. Zoezi la uingizaji
takwimu za rasilimali watu linaendelea katika Mamlaka za Serikali za Mitaa 89
na Sekretarieti za Mikoa 13 ambako mfumo umewekwa. Vifaa vya TEHAMA na mafunzo kwa watumiaji wa
mfumo huu vitaendelea kufungwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizosalia
kupitia Programu ya Kuboresha Mfumo wa Serikali za Mitaa Awamu ya Pili (LGRP
II).
Uendeshaji wa Shule za Msingi na
Sekondari Nchini
41. Mheshimiwa Spika, OWM-TAMISEMI
imeendelea kutekeleza jukumu la kusimamia utoaji wa elimu ya Msingi na
Sekondari kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Ofisi iliziagiza Halmashauri kupitia Sekretarieti za Mikoa kuhakikisha
kwamba watoto wenye umri stahiki wanaandikishwa na kuhudhuria Shule za Msingi
bila kukosa kama inavyoelekezwa na Sera ya Elimu na Mafunzo. Aidha, Halmashauri zilitakiwa zisimamie uwepo
wa madarasa ya elimu ya awali kwenye Shule za Msingi ili watoto wengi zaidi
wapate fursa ya kuhudhuria elimu ya awali kabla ya kuanza darasa la
kwanza. Ofisi ilishirikiana na Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi kufanya ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za ‘Capitation’ katika Halmashauri zake
ikiwa ni pamoja na fedha nyingine zinazopelekwa katika Halmashauri husika. Aidha, Halmashauri zimetakiwa kutumia fedha
wanazopata kwa uadilifu ili kuepuka madeni hasa ya chakula na vifaa vya
kujifunzia.
42. Mheshimiwa Spika,
iko changamoto ya maeneo ya shule hasa mijini kuvamiwa au kwa kutumia mikataba
isiyo halali wafanyabiashara kujenga vibanda vya biashara kuzunguka eneo la shule. Matumizi ya maeneo ya shule yamefafanuliwa
katika Gazeti la Serikali Na. 298 la mwaka 2002 kuwa ni kinyume cha sheria, kanuni na taratibu kufanya
biashara katika maeneo ya shule au kutumia majengo ya shule kwa shughuli za
biashara. Kupitia Bunge lako Tukufu nawaagiza Makatibu Tawala wa Mikoa yote
kuzingatia maelekezo yaliyotolewa na Serikali tarehe 15 Januari, 2010 kuhusu
kudhibiti biashara katika maeneo ya Shule. Aidha, Wakuu wa Mikoa wanatakiwa
kufuatilia suala hili kwa karibu kuhakikisha kuwa biashara hizo zinasitishwa
katika maeneo ya shule. Hata hivyo, suala
la kuwepo kwa vibanda vya chakula, Ofisi yangu kwa kushirikiana na wadau
wengine inaendelea kulifanyia kazi ili kupata utaratibu utakaoonekana unafaa
katika kutoa huduma ya chakula katika shule kwa ajili ya walimu na wanafunzi bila
kuathiri maadili ya msingi ya Shule zetu.
43. Mheshimiwa Spika, vilevile,
viko vibali vya biashara vinavyotolewa na Halmashauri ambavyo vinasababisha
kujengwa kwa majengo ya biashara za nyumba za kulala wageni na baa karibu na
viwanja vya shule. Napenda kutumia fursa hii kupitia Bunge lako tukufu
kuziagiza Halmashauri zote hususan za mijini kusitisha vibali vyote vilivyotolewa
vya kufanya biashara za nyumba za kulala wageni na uendeshaji wa baa katika
viwanja vinavyopakana na maeneo yaliyojengwa shule. Aidha, liko suala ambalo linajitokeza la maeneo ya shule za Msingi na
Sekondari kutokuwa na hati miliki kwa viwanja ambavyo vimejengwa shule
hizo. Hali hii inachangia uvamizi wa
ujenzi wa makazi na biashara katika viwanja vya shule. Halmashauri zote nchini
zinatakiwa kupima viwanja vya shule zilizo katika maeneo yao na kuzipatia hati miliki.
44. Mheshimiwa Spika, ili
kuratibu na kusimamia upatikanaji wa maslahi ya walimu wa shule za msingi na
sekondari kwa kuyaboresha, jumla ya walimu 23,167 waliwasilisha madai
yao Serikalini na kati ya hao 17,682 ni
wa shule za msingi ambao walipelekewa
shilingi 13,040,096,775.00 na walimu 5,485 ni walimu wa shule za sekondari
ambao walipelekewa shilingi 6,169,789,992.00.
Walimu waliopo katika Sekretarieti za Mikoa walipelekewa shilingi 22,789,680.00
na kufanya jumla ya fedha zilizopelekwa kufikia jumla ya shilingi 19,232,676,447.00.
Madai ya malimbikizo ya mishahara ya kiasi cha shilingi 25,643,594,545.43.00
yanalipwa kwenye mishahara ya walimu husika kupitia mfumo wa malipo ya
mishahara ya watumishi wa Umma. Hadi
Aprili 2012 jumla ya shilingi 16,567,655,437.34 zilikuwa zimelipwa. Aidha, jumla
ya shilingi 2,642,231,329.78 zilikuwa zimebaki.
45.
Mheshimiwa
Spika, OWM-TAMISEMI kwa miaka miwili mfululizo iliendelea
kuratibu uendeshaji wa mashindano ya michezo ya Shule za Msingi (UMITASHUMTA) na
Shule za Sekondari (UMISSETA). Michezo iliyoshindaniwa ni riadha, mpira wa
miguu, mpira wa mikono, mpira wa pete, mpira wa wavu, bao, meza, mpira wa
kikapu. Aidha, kulikuwepo mashindano ya taaluma na ubunifu kwa Shule za Msingi.
Mashindano
ya UMITASHUMTA yanahusisha wanafunzi kutoka Tanzania Bara pekee wakati UMISSETA
iliwahusisha wanafunzi kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.
Mpango
wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM)
46. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2011/12, ruzuku ya uendeshaji shule (Capitation grant)
iliyotengwa kwa elimu ya msingi ni shilingi bilioni 50. Hadi kufikia mwezi Mei,
2012 kiasi cha shilingi bilioni 10.1 kimetolewa kwa Mamlaka za Serikali za
Mitaa. Fedha hizo zimetumika kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kufundishia na
kujifunzia, ukarabati wa majengo ya shule, kuendesha mitihani ya ndani na
uendeshaji wa shule za msingi. Aidha, shilingi bilioni 30 ambazo ni sehemu ya
CAPITATION zimetolewa kwa ajili ya ununuzi wa vitabu vya kiada kwa ajili ya
Shule za Msingi.
Fedha za Chenji ya Rada
Mheshimiwa Spika,
Serikali ilipokea fedha za fidia ya ununuzi wa Rada kiasi cha Paundi milioni
29.5 kutoka Serikali ya Uingereza sawa na shilingi bilioni 72.3 za Kitanzania
ambazo zitatumika kuimarisha Elimu ya Msingi Nchini. Kati ya kiasi hicho, ilikubalika shilingi
bilioni 54.2 sawa na asilimia 75 zitumike kununua vitabu vya kiada kwa shule za
msingi na shilingi bilioni 18.1 sawa na asilimia 25 itumike kutengeneza
madawati kwa shule za msingi. Ununuzi wa
vitabu vya kiada utazingatia vitabu ambavyo viliainishwa na Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi mwaka 2009 hata kabla ya fedha za fidia ya rada
hazijajulikana kuletwa nchini ambapo vitabu viwili viwili vya kiada viliteuliwa
kwa kila somo. Kila shule ya msingi nchini itapata vitabu hivyo. Mazungumzo yamefanyika ili kila Mchapishaji
atakayepewa zabuni awajibike kufikisha vitabu hivyo kwenye shule. Ili kuimarisha uwazi vitabu vitapokelewa
shuleni na Kamati ya Shule mbele ya wanafunzi, wazazi na Serikali ya
Kijiji/Mtaa. Mahali kamili kwa
wachapishaji yatatolewa baada ya kupata uthibitisho toka Mikoa na Halmashauti
zote kwamba vitabu vimepokelewa kwa ubora na idadi iliyokubalika.
Mheshimiwa Spika,
shilingi bilioni 18.1 zitatumika kutengeneza madawati kwa shule za msingi.
Kiasi cha madawati yatakayopatikana hakitatosha lakini kitasaidia kupunguza tatizo
kubwa la madawati linalozikabili shule zetu za msingi nchini. Awali ilipendekezwa kuwa madawati hayo
yanunuliwe na kusambazwa kwenye Halmashauri zilizokuwa na upungufu mkubwa wa
madawati yaani upungufu unaofikia madawati 100,000 au zaidi. Hata hivyo, Serikali imetafakari tena na
kuona kwamba kigezo cha upungufu mkubwa pekee si kigezo bora cha kutumia katika
kugawa madawati. Kutokana na uamuzi huu,
kila Halmashauri itapata mgao wa madawati.
Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya
Sekondari (MMES)
47.
Mheshimiwa Spika, kazi za Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari Awamu
ya Pili (MMES II) zilizotekelezwa katika mwaka 2011/12 ni kufanya uchambuzi
yakinifu wa shule 264 ambazo zitafanyiwa ukarabati mwaka 2012/13; kuandaa
moduli za mafunzo ya Bodi za Shule na Waratibu Elimu Kata ili kusimamia
uendeshaji na uratibu wa elimu ya Sekondari.
Mafunzo yataanza katika mwaka wa fedha 2012/13. Maafisa Elimu wa Mikoa 25, Maafisa Elimu Taaluma wa Mikoa 25, Maafisa Elimu wa
Sekondari wa Halmashauri 133, Maafisa Elimu Taaluma 133 wa Halmashauri na Wakuu
wa Shule 3,435 wa shule za Serikali na zisizo za Serikali walipata mafunzo
kuhusu usimamizi na uendeshaji wa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari
Awamu ya II (MMES II).
48.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2011/12 Serikali ilitenga jumla ya
shilingi bilioni 22.9 kwa ajili ya uendeshaji wa Shule za Sekondari. Hadi
kufikia Machi, 2012 jumla ya shilingi bilioni 7.6 zimetolewa na kupelekwa
kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya Capitation ya shule ikiwa ni
pamoja na ununuzi wa vitabu vya kiada na vifaa vya maabara.
49. Mheshimiwa Spika, kazi
zilizopangwa kutekelezwa katika mwaka 2012/2013 ni kufanya ukarabati wa shule
264 zilizoanishwa; Kutoa mafunzo kwa Bodi za Shule, kuendesha michezo ya UMISSETA;
Kushiriki katika kufuatilia utoaji wa elimu ya Sekondari katika Mikoa na
Mamlaka za Serikali za Mitaa na kuchukua hatua stahiki.
Programu
ya Usimamizi Shirikishi wa Misitu na Ardhi Oevu
50. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2011/12 Programu ya Usimamizi Shirikishi wa Misitu (PFM)
ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya kuendeleza usimamizi
shirikishi wa misitu katika baadhi ya Halmashauri za Mikoa ya Morogoro, Iringa
Njombe, Mbeya, Lindi Tanga, Ruvuma, Rukwa, Lindi, Kigoma, Mtwara, Mara,
Shinyanga, Dodoma, Pwani na Kagera chini ya ufadhili wa DANIDA na Finland. Kiasi
cha fedha kilichotolewa hadi Machi 2012 ni shilingi 490,493,000.00. Fedha hizo
zimetumika kuratibu utoaji wa elimu kwa jamii kuhusiana na hifadhi ya misitu na
mazingira.
51. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2011/12 Programu Shirikishi ya Usimamizi wa Ardhi Oevu
iliidhinishiwa shilingi 758,600,000.00. Kati ya fedha hizo shilingi 158,600,000.00
ni kwa ajili ya uratibu na shilingi 600,000,000.00 zimepelekwa katika Mamlaka
za Serikali za Mitaa zinazotekeleza Programu.
Programu hiyo inatekelezwa katika Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mikoa
ya Arusha, Iringa, Njombe, na Mbeya. Kazi zilizotekelezwa katika Mamlaka hizo
ni pamoja na kufanya mapitio ya mwongozo wa usimamizi wa fedha na utekelezaji
wa programu na kuandaa mafunzo kuhusu mwongozo kwa watendaji wa Mamlaka.
Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Kilimo (ASDP)
52. Mheshimiwa Spika, kwa
kutumia bakaa ya fedha ya mwaka 2010/11 na fedha za 2011/12, Halmashauri
zimeendelea na uboreshaji wa miundombinu ya masoko ya mazao kwa kujenga jumla
ya masoko 84 kwa wanufaika 197,750, barabara za maeneo ya Vijijini (feeder
roads) zenye urefu wa km. 263 na madaraja madogo 25 kwa ajili ya kurahisisha
usafirishaji wa mazao na pembejeo yamefanyiwa ukarabati. Aidha, kwa upande wa miundombinu
ya mifugo, jumla ya malambo 27 yamejengwa kwa wanufaika 47,837. Vilevile Mamlaka za Serikali za Mitaa
zimeendelea kuvijengea uwezo vikundi mbalimbali vya wakulima kiuchumi katika
maeneo yao na jumla ya wanufaika 17,315 wamepatiwa mafunzo ya uboreshaji wa
bidhaa zinazotokana na kilimo ili kuwa na uhakika wa masoko. Pia jumla ya
mashamba darasa 4,542 na vikundi 14 vya watumia maji (Water User Association)
vimepatiwa mafunzo ya mbinu bora za uzalishaji mazao ya kilimo na mifugo kwenye
Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Mkakati wa Kufufua na
Kuendeleza Sekta na Viwanda vya Ngozi
53.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa
fedha 2011/12 Jumla ya shilingi 677,000,000.00 zimepelekwa
katika Mamlaka za Serikali za
Mitaa 65 kwa ajili ya kutekeleza
mkakati wa kufufua na kuendeleza Sekta ya Viwanda vya Ngozi. Kila
Halmashauri imepangiwa kutumia jumla ya shilingi
10,415,384.00 zinazotekeleza mkakati
huo. Vikao vya uhamasishaji, mafunzo, warsha na ziara za mafunzo vilifanyika kwa
wadau wa zao la ngozi ikiwa ni pamoja na
Wafugaji, Wachunaji, Wawambaji, Wasindikaji, Wachambuzi wa Madaraja na Wafanyabiashara,
Madiwani, Maafisa Ugani, Wakuu wa Idara, Viongozi wa Vijiji na Vitongoji. Uhamasishaji huu umeleta ufahamu juu ya
umuhimu wa zao la ngozi na umechangia katika ongezeko la ubora na biashara ya
zao la Ngozi. Vilevile, vimeanzishwa vikundi
vya ujasiriamali katika usindikaji na utengenezaji wa bidhaa za zao la Ngozi na uundaji wa vyama vya wadau wa
zao la ngozi unaoendelea kufanyika katika Halmashauri zote zinazotekeleza
Mkakati .
54.
Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Machi, 2012
jumla ya ngozi za Ng’ombe zilizokusanywa zilikuwa ni 475,639, ngozi za Kondoo ni 94,166 na ngozi za Mbuzi ni 322,249. Katika mwaka wa fedha 2012/13 jumla ya
shilingi 855,900,000.00 zimetengwa
kwa ajili ya Mamlaka za Serikali za Mitaa 65 Tanzania Bara zinazotekeleza Mkakati huu na jumla ya shilingi
25,000,000.00 zimetengwa kwa ajili ya uratibu.
Programu
ya Mfuko wa Pamoja wa Afya (Health Basket Fund)
Mheshimiwa
Spika, Serikali kupitia Mfuko wa pamoja wa Afya
katika kipindi cha fedha cha mwaka 2011/2012 imepeleka jumla ya Shs 80.99
bilioni katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa huduma katika zahanati 4,105,
vituo vya afya 457 na hospital 112 zinazomilikiwa na serikali ili kuimarisha
huduma za tiba na Afya kwa ujumla. Aidha, kupitia mfuko huu shughuli zifuatazo
zimetekelezwa: ununuzi wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi, kujenga uwezo kwa
watumishi wa sekta ya afya wa ngazi zote, usimamizi, ufuatiliaji na uratibu na
kuimarisha muundo wa sekta ya afya. Vile vile mfuko huu umesaidia kuimarisha
utaratibu wa rufaa kutoka vituo vya afya/zahanati kwenda Hospitali za Wilaya na
usambazaji dawa, chanjo na vitendanishi. Mfuko huu pia umetumika kuhakikisha
watumishi wanakuwepo katika vituo vya kutolea huduma masaa yote na upatikanaji
wa maji, umeme na usafi wa mazingira
Taasisi
na Mashirika
Chuo
cha Serikali za Mitaa Hombolo
55. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2011/12, Chuo cha Serikali za Mitaa HOMBOLO kimeendelea na
mipango yake ya kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi. Katika kipindi hicho Chuo
kiliweza kuanzisha kozi mpya nne hivyo kufanya jumla ya kozi zinazotolewa mpaka
sasa kuwa nane kutoka nne za awali. Kozi mpya zilizoanzishwa zinalenga kuongeza
wataalamu wa fani ambazo zitasaidia kuimarisha utendaji wa kazi katika Mamlaka
za Serikali za Mitaa. Kozi hizo ni:- Astashada ya Maendeleo ya Jamii, Astashahada
ya Usimamizi wa Rasilimali Watu, Stashahada ya Maendeleo ya Jamii na Stashahada
ya Usimamizi wa Rasilimali Watu.
56. Mheshimiwa Spika, udahili
wa wanafunzi pia uliongezeka kutoka wanafunzi 1,389 mwaka 2010/11 hadi kufikia
wanafunzi 2,286 katika mwaka wa masomo 2011/12. Idadi hii ni ongezeko la wanafunzi
897 sawa na asilimia 65 ya wanafunzi waliodahiliwa mwaka wa masomo 2010/11. Chuo
kiliendesha mafunzo ya muda mfupi kwa Wenyeviti wa Vijiji 32 vya Halmashauri za
Mbinga na Maafisa Watendaji wa Vijiji 20 wa Halmashauri
za Misenyi, Magu, Karagwe na Ukerewe, Wakuu wa Idara kutoka Halmashauri ya Wilaya
ya Nzega (Maafisa 6) na Madiwani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi.
57. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa fedha 2011/12 Chuo kilipewa kiasi cha shilingi bilioni 1.5 ikiwa ni ruzuku
ya miradi ya maendeleo. Kiasi cha shilingi 426 milioni kimetumika kulipia
sehemu ya fidia ya eneo lililochukuliwa na Chuo kwa ajili ya upanuzi, shilingi milioni
300 zitatumika kujenga nyumba mbili (2) za watumishi, shilingi 700 zitatumika
katika mradi wa ujenzi wa kituo cha afya na sehemu ya kiasi kilichobakia shilingi
75 milioni kimetumika kuweka samani katika nyumba mpya 15 za watumishi (daraja
la A na B).
58. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2012/13, Chuo kimetenga shilingi milioni 650 kwa ajili ya
kulipa fidia. Serikali itaendelea kukiimarisha Chuo kwa kuongeza idadi ya
wataalamu mbalimbali ili kiweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu.
Wakala wa
Usafiri wa Haraka (Dar es Salaam Rapid Transit - DART)
59. Mheshimiwa
Spika, usafiri wa haraka Dar es Salaam (DART) ni Mkakati wa
Serikali wa muda mrefu utakaotumia mabasi makubwa kupitia njia maalum katika Jiji
la Dar es Salaam ili kupunguza msongamano. Usanifu wa kina wa mradi awamu ya pili
(Kilwa Road) na ya tatu (Nyerere Road) umekamilika. Ujenzi wa Miundombinu awamu
ya kwanza katika barabara ya Morogoro umeanza kutekelezwa. Wakala unakamilisha usanifu wa kina wa mfumo wa
DART awamu ya 2 na 3 yenye urefu wa kilomita 42.3.
60. Mheshimiwa Spika,
gharama za ujenzi wa mfumo huu awamu ya kwanza kupitia Benki ya Dunia ni dola
za Marekani milioni 225.37 na Serikali ya Tanzania hadi sasa imechangia shilingi
bilioni 11.5. Sekta Binafsi inatarajiwa kuwekeza kiasi cha Dola za Marekani
milioni 40.9. Aidha, hivi sasa mradi
umefikia hatua muhimu ya utekelezaji baada ya kusainiwa kwa mkataba kati ya
Kampuni ya Ujenzi ya STRABAG kutoka Ujerumani na Serikali tarehe 22 Desemba 2011.
Wakala pia umelipa fidia awamu ya kwanza katika kituo cha mabasi Ubungo kwa
kutumia shilingi milioni 500 zilizokuwa zimetengwa mwaka 2011/12. Matarajio kwa
sasa ni kwamba ifikapo mwaka 2014 sehemu kubwa ya mradi itakuwa imekamilika na
kuanza kutumika.
Mfuko wa Pensheni wa Serikali za Mitaa (LAPF)
61.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2011/12, Mfuko uliandikisha wanachama wapya 10,195 kati ya lengo la kuandikisha wanachama
10,216. Hadi Machi 2012, Mfuko
ulikusanya michango ya wanachama shilingi bilioni 66 kati ya lengo la kukusanya
shilingi bilioni 87.5. Katika lengo la uwekezaji,
Mfuko uliwekeza shilingi bilioni 111.46 kati ya lengo la kuwekeza shilingi bilioni
163.83. Vilevile, katika kipindi hicho Mfuko ulipata shilingi bilioni 20.37
kutokana na uwekezaji uliokuwepo kati ya matarajio ya kupata shilingi bilioni
43.81 kwa mwaka.
62.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/13 Mfuko unategemea kuandikisha wanachama wapya 11,591 na kufanya idadi ya
Wanachama kuongezeka kutoka 92,269 Juni
2012 hadi 103,860 ifikapo Juni 2013. Mfuko umelenga kukusanya
shilingi bilioni 107.66 kutokana na Michango ya wanachama na
kuwekeza shilingi bilioni 196.74 kwenye vitega uchumi mbalimbali na
kulipatia Shirika mapato ya shilingi bilioni 42.67. Pia Mfuko unategemea kutumia
kiasi cha shilingi bilioni 35.27 kwa
ajili ya malipo ya mafao. Aidha, Mfuko katika kutekeleza Sheria mpya ya Mamlaka ya
Hifadhi ya Jamii, umepanga kuendelea na utafiti wa kubainisha utaratibu bora wa
kutoa mafao ya elimu na njia mwafaka ya kupanua wigo kwa sekta isiyo rasmi.
Shirika
la Elimu Kibaha
63.
Mheshimiwa
Spika, katika kutekeleza
malengo yake, Shirika la Elimu Kibaha kwa mwaka 2011/12 limeweza kutoa Elimu na
malezi bora kwa wanafunzi 2,920. Wanafunzi 915 walipata elimu ya msingi
(wavulana 447 na wasichana 468), Wanafunzi 1,532 walipata Elimu ya Sekondari Kidato
cha Kwanza hadi cha Nne (Wavulana 855 na Wasichana 677) na wanafunzi 373 ambao
wote ni Wavulana walipata Elimu ya Sekondari Kidato cha Tano na Sita. Aidha,
vitabu 914 vilinunuliwa, Walimu 126 walilipwa posho ya
nauli wakati wa likizo, walimu 26 walikuwa wakiendelea na masomo katika ngazi
ya Shahada na Walimu 11 waliajiriwa.
Shirika lilitoa huduma ya Maktaba kwa wadau 34,112, wanaume 27,706 na wanawake
7,406.
64.
Mheshimiwa Spika, Elimu ya nadharia na vitendo kupitia Chuo cha Maendeleo
ya Wananchi ilitolewa kwa
wanachuo 408 (wavulana 245 na wasichana 163). Mafunzo yaliyotolewa ni Kilimo na
Mifugo, Ujenzi na Useremala, Ushonaji na Upishi, Ufundi wa Magari, Uundaji na
Ufuaji Vyuma na Umeme wa Majumbani. Mafunzo ya muda mfupi yalitolewa kwa wadau
255. Mafunzo hayo yalikuwa ni udereva,
ujasiriamali, kilimo cha bustani, kilimo cha uyoga, kutengeneza tofali na
kuchakata ngozi.
65.
Mheshimiwa Spika elimu ya kinga na tiba kupitia Hospitali Teule ya
Tumbi ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani ilitolewa kwa wagonjwa 247,985. Kati yao waliolazwa ni 50,949 (wanawake
33,798 na wanaume 17,151) na wa nje walikuwa 197,036 (wanawake 105,246 na
wanaume 91,790). Pia hospitali ilihudumia majeruhi wa ajali za barabarani
2,724.
66. Mheshimiwa
Spika, Shirika pia
liliendelea kupambana na janga la UKIMWI. Katika mwaka wa fedha 2011/12,
wagonjwa 6,168 (wanaume 2,845 na wanawake 3,323) walipewa ushauri nasaha na
kupimwa UKIMWI. Wagonjwa 1,051 walisajiliwa katika Kliniki ya kutoa
huduma kwa wanaoishi na virusi vya UKIMWI (CTC). Ujenzi wa upanuzi wa Hospitali ya Tumbi awamu ya pili
inayojumuisha ujenzi wa vyumba vya upasuaji, ofisi na sehemu ya mapokezi
uliendelea.
Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa
67.
Mheshimiwa Spika, jukumu la Bodi ya Mikopo ya
Serikali za Mitaa ni kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwenye Mamlaka za
Serikali za Mitaa kwa ajili ya kutekeleza
miradi ya maendeleo. Hadi Aprili, 2012
mikopo ya jumla ya shilingi bilioni 1.028 imetolewa kwenye Halmashauri tatu za
Lushoto, Mbinga na Mtwara Mikindani na kufanya mikopo yote iliyotolewa kufikia
jumla ya shilingi bilioni 5.5 ikilinganishwa na maombi yaliyowasilishwa ya
jumla ya shilingi bilioni 25.1 tangu Bodi ianzishwe.
68.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi
hicho michango ya Akiba ya jumla ya shilingi milioni 322.4 imewasilishwa kati ya shilingi bilioni 1.1
zilizokadiriwa na kufanya michango yote ya Akiba kufikia jumla ya shilingi bilioni
4.9 ikilinganishwa na kiasi kilichopaswa kuchangwa cha jumla ya shilingi bilioni
5.6. Kuhusu Mikopo na riba, jumla ya shilingi milioni 279.7 zimerejeshwa na
kulipwa kati ya shilingi milioni 958 zilizokadiriwa. Uwasilishaji wa Michango
na marejesho ya mikopo umekuwa siyo wa kuridhisha. Hadi tarehe 15 Aprili, 2012,
Bodi inazidai Halmashauri 64 jumla ya shilingi bilioni 3.1 kwa viwango tofauti
kutokana na Michango ya Akiba (MCR) na Mikopo pamoja na Riba.
69.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza kuchukua hatua
za kuufanyia marekebisho muundo wa Bodi.
Matarajio ya marekebisho haya ni kuwa na chombo cha fedha cha Serikali za
Mitaa kilichoimarika na kinachojitegemea
kwa kuwa na uwezo wa kusimamia na kuendesha shughuli zake kwa asilimia 100
katika nyanja zote za utumishi, kifedha, na tekinolojia ya habari na
mawasiliano.
HITIMISHO
70.
Mheshimiwa Spika, OWM-TAMISEMI inapenda
kuwashukuru wadau wote ilioshirikiana nao katika kutekeleza majukumu yake kwa
mwaka 2011/12 na inatoa rai waendelee kutoa ushirikiano katika kutekeleza
majukumu ya mwaka 2012/13.
No comments:
Post a Comment