Na:
Gabriel Athumani.
DODOMA.
Mwanafalsafa wa zamani nchini Ugiriki,
Plato, ni miongoni mwa binadamu waliojaliwa kuwa na uwezo wa kufikiri, lakini
akitumia zaidi nadharia za mwalimu wake, Socrates.
Alipokuwa anaangalia juu ya dola
wakati ule, aliamini kuwa dola ambayo inaweza kufanya mambo yake vizuri,
inaweza kupatikana kama wakiwapo watu makini wa kuingoza.
Akaendelea
kusema; na kwa kuwa njia kuu ya mafanikio ni hekima ya kiongozi ambaye anafanya
maamuzi kwa ajili ya jamii nzima, basi jamii nzuri itapatikana tu pale Wafalme
watakapokuwa Wanafalsafa au Wanafalsafa wamefanywa kuwa Wafalme.
Nimetumia
nukuu hii ikiwa ni mwendelezo wa mjadala wangu wa wiki iliyopita nilipojadili
kuhusu baadhi ya wanasiasa kujiona wanajua kila kitu kuliko wengine. Kujiona ni
wababe wasioweza kuguswa na yeyote na kwamba wanaweza hata kuropoka chochote na
wasihojiwe.
Nimetumia
maneo hayo ya Plato kuelezea umuhimu wa hekima katika kuongoza watu, umakini wa
viongozi ili uwe na Taifa zuri na uwezo wa kiongozi kuchambua mambo kwa kutumia
elimu na ufahamu wake.
Katika
wiki iliyomalizika tumeshuhudia mambo yanayofanana kidogo na mjadala wangu wa
wiki iliyopita, na yanayolandana na muono wa mwanafalsafa, Plato. Katika habari
za magazeti ya hapa nchini, moja wapo iliyokuwa imebeba uzito ni ile Chadema
kumwandikia barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho
Kikwete. Kuna magazeti yalikuwa na kichwa cha habari “Chadema ‘wamlima’ barua
JK”.
Habari
nyingine, ni ile ya Chadema kumsusia Msajili wa Vyama vya Siasa pamoja na ile
ya Chadema kuhamasisha maandamano Iringa. Lakini kubwa kuliko yote ni pale
Mchumba wa Dk. Wilbroad Slaa, Katibu Mkuu wa Chadema, Josephine Mushumbusi
alipoibua tuhuma nzito akidai kuna mpango wa kumuua mumewe kwa sumu au uchawi!
Habari
hizo zote, ukisoma kwa umakini, utagundua
jambo moja linalofanana na umuhimu wa maneno ya Plato niliyoyagusia hapo
juu.
Tukianza
na ile ya Chadema kumwandikia barua Rais. Unachoweza kukiona haraka haraka ni
kukosekana kwa hekima, na umakini katika kufikia uamuzi na kutoa tamko kama
lile. Angalia lugha ya kibabe inayotumika kumtisha na kumwamrisha Rais, angalia
mambo yaliyosababisha tamko lile.
Unaweza
kujiuliza, wao ni akina nani mpaka wafikie hatua ya kumtaka Rais afanye
watakavyo na si watakavyo Watanzania au atakavyo yeye aliyepewa mamlaka na
Katiba kufanya uteuzi na kufukuza. Mbaya zaidi, amri zote hizo kwa Rais
zinaishia kwa masharti ya kumtisha ati; “Iwapo Serikali haitazingatia, Chadema
kitawaongoza wananchi kwa njia ya
kidemokrasia ikiwamo maandamano kuishinikiza”. Ni kukosa hekima na umakini.
Kama
hiyo, haitoshi Chadema hao hao, wiki iliyopita walisusia semina iliyokuwa
imeandaliwa na John Tendwa, Msajili wa Vyama vya Siasa iliyovishirikisha vyama
vya siasa na wadau wengine. Wameapa kutoshirikiana naye mpaka pale Rais
atakapomuondoa katika nafasi aliyonayo.
Hivi,
kama kweli busara ilitumika, kumsusia Tendwa ambaye ndiye anayefahamika
kisheria, halafu wakati huo huo, wanadai wataendelea kuiheshimu Sheria ya Vyama
vya Siasa, akili ya kawaida inaonyesha kuna mapungufu makubwa katika safu ya
uongozi ya Chadema. Msajili wa Vyama vya Siasa anatajwa kwenye Sheria ya Vyama
vya Siasa ingawa si kwa jina la Tendwa, lakini aliyepo kwa mujibu wa Sheria
hiyo ndiyo huyo. Sasa wanaiheshimu sheria ipi. Hekima ni muhimu katika uongozi.
Aidha,
mchumba wa Dk. Slaa, Josephine naye amekuja na kali nyingine kama iliyowahi
kutolewa na Kamati Kuu ya Chadema hivi karibuni. Josephine ambaye katika habari
hiyo inadaiwa yupo nje ya nchi, amenukuliwa akiandika kuwa kuna vikao vya watu
ndani ya Serikali vyenye lengo la kutaka kummaliza Dk. Slaa kwa njia yoyote
ile.
Amenukuliwa
“Wanaamini kwamba Dk. Slaa ndiye mzizi wa Chadema na anaweza kuiangusha CCM
2015. Wameona mazingira ya kuchakachua 2015 ni magumu sana”. Pia katika taarifa
yake hiyo, Josephine anahusisha sumu na uchawi kuwa vitatumika katika harakati
hizo za kummaliza ‘mumewe’.
Anasema;
“Kwenye kikao chao cha kidhalimu, mmoja wao akapendekeza matumizi ama ya uchawi
au sumu inayoua taratibu. Huyu aliyependekeza anahofia kuwa njia yoyote
itakayofanana na nyingine italeta kelele na dunia nzima itagundua. Anajaribu
kuwashawishi wenziwe waachane na hiyo, isipokuwa watumie njia hizi mbadala;
sumu au uchawi.”
Habari
zote hizo hapo juu kwa muhtasari utagundua jinsi watu hao walivyokosa hekima na
umakini katika matamshi yao. Kwa wenzangu kutoka makundi mbalimbali kati jamii
hii ya Kitanzania, tulisaidie kundi hili la Chadema!
Nasema
tulisaidie kwa sababu pamoja na wengi wao kuwa na umri kama wangu, wenye akili
isiyochoka, lakini wanaonekana stamina za kisiasa hazipo. Hakuna wanachowaza ni
kuitishia Serikali kwa maandamano. Mara Mbunge wa Iringa Mjini anahamasisha
wananchi waandamane, kumshinikiza Rais kumuondoa Kamanda wa Polisi wa Mkoa,
Michael Kamuhanda!
Haiwezekani
kila kukicha, habari ni za kumtishia Rais, Waziri Mkuu, Waziri, Mkuu wa Mkoa kisa, demokrasia ya upinzani.
Hapana. Hakuna nchi wala Serikali ambayo kuanzia Januari mpaka Desemba kundi
fulani lipo kuiyumbisha ili ishindwe kufanya kazi zake. Hakuna Serikali
inayoweza kufanya kazi kwa matamko ya kuiamrisha kutoka vyama vya siasa.
Hakuna
Rais anayefanya kazi kwa kuamrishwa na Kiongozi au Kamati Kuu ya chama
asichokiwakilisha. Hata kama Serikali hii ingekuwa ya Chadema, isingefanya kama
inavyotaka sasa viongozi wa Serikali ya CCM wafanye.
Tuwasaidie
akina Freeman Mbowe, Dk. Slaa, John Mnyika na wengine ndani ya Chadema kuwa
“ukitaka mbio, agana na nyonga”. Wasijidanganye kwa malengo ya muda mfupi ya
kutaka tu kuingia Ikulu. Mikakati inayofanyika sasa inajionyesha wazi si ya
kutaka kuongoza nchi bali kuingia Ikulu, wakifika huko ndiyo watajua wenyewe
biashara watakayoifanya.
Nasema
haya kwa sababu mbili kubwa, mosi; Viongozi wa Chadema wanatumia raslimali
nyingi za chama na nje ya chama kuliunda kundi la Watanzania wabishi, wapenda
maandamano, wapinga kila kitu hata kama ni kizuri na wakaidi wa amri halali za
Serikali na dola. Pili wanategeneza kundi la Watanzania waongo, wanafiki,
wazushi, na waropokaji.
Makundi
hayo hapo juu yanaundwa kwa kiasi kikubwa na vijana. Vijana ambao tayari
wameiva kwa yote niliyoyaorodhesha. Wajue kuwa, hakuna namna Serikali
itakayoundwa na Chadema kama ikitokea, inaweza kuyabadilisha makundi hayo
mawili. Haitawezekana kwa sababu, vijana hawa na wengine hawawashabikii viongozi
wa Chadema kwa sababu wao handsome, au warembo.
Hasira
waliyoijaza kwa makundi haya haitakwisha wakiingia madarakani, kwani wameziwekeza
katika matarajio ya kesho. Kama leo anaichukia CCM kwa sababu umemwambia hakuna
ajira, kesho ukiingia madarakani, bado kukawa hakuna ajira, unatulizaje hasira
yake!
Kwa
jinsi walivyofuzu somo la kuandamana kwa alama za juu, utawazuia vipi kufanya
maandamano kudai kima cha chini cha mshahara kuwa milioni mbili? Jamii
iliyofuzu yote yanayofundishwa sasa na viongozi wa Chadema ni ya Watanzania.
Hatutegemei Chadema ikiingia madarakani, itakwenda kuchukua Wachina ndio
wawatawale.
Ni
Watanzania wale wale ambao vijana wengi wako mijini wakifanya biashara ndog
ndogo (Machinga) ambao Chadema imewafundisha kuzomea viongozi hata pale
wanaposhauriwa mambo yenye manufaa kwao.
Ni
vijana wale wale wanaosoma katika shule zetu za Sekondari za Kata mnazoziponda
leo, ambazo hawatazitaka tena kwani mlishawaambia hazifai. Ni watanzania wale
wale, watakaougua, ambao watataka kila zahanati iwe na mashine ya X-Ray, kwa
sababu mlisema inawezekana.
Ni
watanzania wale wale, wanaonunua mfuko mmoja wa sementi kwa Sh 20,000 leo,
ambao Chadema ikiingia madarakani hawataelewa kama haitauzwa kwa Sh.5,000,
lazima wataandamana. Wamefuzu shughuli hiyo. Na ni Polisi wale wale wanaotuhumiwa
kuua kwenye mikutano ya Chadema ndiyo watalinda maandamano.
Baadhi
ya wanaharakati, wasomi, waandishi wa habari na vyombo vya habari wanaoshabikia
yanayoandaliwa sasa na Chadema, wasaidieni viongozi wake kwani, ukipanda bangi
utavuna bangi.
Wasaidieni
wajue kuwa wao si wajuzi wa kila kitu, wasikilize na wajifunze namna ya
kuwaanda wananchi kupokea utawala wao wakiwa wavumilivu, wamoja, na wenye
subira. Wasaidieni kuwaambia kuwa wasitengeneze njia za mkato kuingia
madarakani, bali wajipange kujua namna ya kuingia madarakani.
Wasaidieni
kujua kuwa, wakiingia madarakani hawatashangiliwa kila wapitako, watazomewa na
kurushiwa mawe kama walivyowafundisha kufanya hivi sasa. Watafanyiwa vurugu,
watatukanwa, wataandikwa vibaya, kupingwa kama wafanyavyo wao.
Chadema
kama cha siasa kinachoipa changamoto CCM kwa staili ya kuidhoofisha kwa mbinu
chafu, zikiwamo zile za uzushi kama unaofanywa sasa wa kusingizia viongozi wa
Serikali na vyombo vya dola kupanga mikakati ya kuwadhuru, kinajitengenezea
hatima watakayokuja kuijutia.
Watakwenda
vijijini kwa chopa, wananchi watazishangaa, watawashangaa pia akina Dk. Slaa, watagawa
kadi mithili ya vipeperushi vya maelezo ya waganga wa kienyeji, watawatukana
viongozi wao, watapata burudani ya uongo na uzushi, lakini mwisho wa siku, kila
mmoja anatafakuri juu ya maisha yake.
Kutokana
na kukosa hekima inayosaidia kujenga jamii nzuri, tumesikia jinsi ufisadi wa
kutisha katika Halamsahauri ya Manispaa ya Moshi inayoongozwa na Chadema,
ulivyofichuliwa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama. Na kwa
kudhirisha jinsi wasivyo makini, Meya wa Manispaa hiyo, anatamka kutoshirikiana
na Mkuu wa Mkoa kwa madai ati anatumika kisiasa.
Hivi
kweli, msafara wa watu 58 mnakwenda kujifunza Kigali kwa kutumia Sh. 200
milioni kuna tija kweli hapo? Katika hali ya kawaida na haiingii akilini kuwa
watu 58 wanakwenda mafunzoni kwa mpigo, huo ni wizi wa fedha za walipa kodi tu
na hakuna maelezo mengine.
Na
jambo hili, kama lingefichuliwa kwenye Halmashauri inayoongozwa na CCM, albamu
nyingine ya ufisadi ingekuwa inauzwa nchini. Ungeimbwa majukwaani, kwenye
magazeti, midahalo isiyo na tija na mitandao ya kijamii. Hongera sana Mkuu wa
Mkoa, kaza uzi hawana namna ya kuendesha mambo yao bila Serikali kujua kwani
fedha ulizookoa si za Chadema, ni za umma.
Nafahamu
Waafrika tuna hulka ya kudandia mambo bila ya kuyapima na hasa tukihamasishwa
na nguvu kutoka nje. Tukiambiwa tufanye mabadiliko, hata kama hatupewi sababu
za msingi, tumo! Tunashabikia mambo ambayo hatuyajui kabisa. Mfano ni kama ule
wa Uganda, pale Idd Amin alipoipindua Serikali ya Milton Obote.
Waganda
wakiamini kuwa Idd Amin ni mkombozi, walimpongeza na waliyashangilia mapinduzi
yale ambayo Mganda yoyote, ukimuuliza leo kama yalikuwa na ulazima wowote,
ataishia kusikitikia yaliyokuja kutokea baada ya hapo.
Libya
yamefanyika mapinduzi yaliyomuua Kanali Muammar Gaddaf, Misri yametokea
mapinduzi yaliyomg’oa Hosni Mubarak, Tunisia kadhalika. Mapinduzi haya yote
barani Afrika yameshabikiwa hata hapa nchini kwetu, lakini chanzo chake na
kufanikiwa kwake ni kutokana na nguvu za nje ya nchi hizo.
Tumeshuhudia
jinsi majeshi ya NATO yalivyoshiriki kule Libya. Lakini Waafrika hatujiulizi
kulikoni NATO na Gaddaf. Yalitaka kutokea kule Zimbabwe, Rais Robert Mugabe
alivyowekewa vikwazo na nchi za Wazungu kulazimishwa akubaliane wanachotaka
kuhusu kibaraka wao.
Chadema
kama chama cha siasa kina muda na nafasi ya kufanya siasa za kistaarabu. Si uhodari
wala sifa kiongozi kuwa muongo, mzushi kwa sababu tu unataka umaarufu.
Kujisingizia kutaka kuuawa kisha hutaki kutoa taarifa zako kwenye vyombo vya
dola ni kutafuta umaarufu wa kitoto.
Kama
viongozi hawatashituka na kuendelea kucheza “CD ya ufisadi” ambayo imechuja,
chama kitajikuta kikija na sababu za vichekesho kwa wanachama wake pale
watakapokuwa wanashindwa kwenye uchaguzi.
Watanzania
wanataka kusikia au kuona mikakati ya kuwaletea maendeleo na kuondosha kero
zao. Hawahitaji kuongezewa kero ya maandamano, wala kusikiliza hadithi za
kutunga. Kama nilivyosema Chadema wana muda na nafasi waachane na kutengeneza
mabomu ambayo yanaweza kuwalipukia wenyewe. Hata kama wao wangekuwa madarakani,
wanayoyafanya sasa ndiyo watakayofanyiwa.
Mungu
Ibariki Tanzania.
No comments:
Post a Comment